MWANDISHI WETU, MUFINDI

mtwarapressclub@gmail.com

Wakala ya Barabara za Vijijini na Mijini (TARURA) Mkoa wa Iringa, inaendelea na ujenzi wa barabara ya Iyegeya- Lulanda yenye urefu wa Km 10.4 kwa kiwango cha lami kwa kutumia Teknolojia mbadala ya ECO Roads ikiwa ni utekelezaji wa malengo ya Serikali ya kupunguza gharama za ujenzi na matengenezo ya barabara.

Akizungumza wakati wa ziara maalum ya ukaguzi wa mradi huo Septemba 21, 2023, Meneja wa TARURA Mkoa wa Iringa Mhandisi Makori Kisare ameeleza kuridhishwa na kasi ya ujenzi wa mradi huo uliofikia asilimia 50 ya utekelezaji na kubainisha kuwa matarajio makubwa ni kukamilika kwa mradi huo ndani ya muda uliopangwa.

“Kasi ya utekelezaji wa mradi huu ni kubwa na matarajio ni kwamba mradi huu utakamilika kwa wakati na kuwanufaisha wananchi ili waweze kusafiri na kusafirisha mazao yao kwa urahisi kutoka eneo la Sawala hadi Lulanda”, alisema Mhandisi Makori.

Barabara hiyo ya Iyegeya kwenda Lulanda tayari Mkandarasi anaendelea na hatua mbalimbali za utekelezaji na ujenzi wake unatarajia kukamilika ifikapo Agosti 2024.

Barabara ya Iyegeya- Lulanda inajengwa ikiwa ni mwendelezo wa barabara ya Sawala-Mkonge-Iyegeya kilomita 30 ambazo tayari zilishajengwa kupitia mradi wa Agri-Connect.

Check Also

WANANCHI WA MABOGINI WANUFAIKA NA MRADI WA RISE

MOSHI-KILIMANJARO Wananchi wa kijiji cha Mabogini, kata ya Mabogini, wilayani Moshi Mkoani…